Top News


MADIWANI MSALALA:Tumeridhishwa na Utendaji wa RUWASA katika Miradi ya Maji.

NA ANTHONY SOLLO KAHAMA.

Mwenyekiti wa Halmashauri ya Msalala Mh Mibako Mabubu akizungumza jambo katika Kikao cha Baraza la Halmashauri ya Msalala lililofanyika katika Ukumbi wa Halmashauri hiyo na kupendekeza kuidhinishwa matumizi ya Sh Bil 10.2 
Pichani ni Kaimu Meneja wa RUWASA Pastory Mnyeti akizungumza na waandishi wa Habari mara baada ya Kikao cha baraza la Madiwani wa Halmashauri ya Msalala kilichopendekeza bajeti ya matumizi ya Sh Bil 10.2 kwa mwaka wa fedha 2024/25. 


pichani ni muonekano wa Jengo la Kisasa la Halmashauri ya Msalala Wilaya ya Kahama Mkoani Shinyanga.


Pichani ni moja ya Tenki la Maji lililojengwa katika moja ya Miradi inayotekelezwa kwa wananchi wa Halmashauri ya Msalala Wilaya ya Kahama Mkoani Shinyanga.
Picha zote na ANTHONY SOLLO SHINYANGA.

BARAZA la Madiwani wa Halmashauri ya Msalala Wilaya Kahama Mkoani Shinyanga limependekeza na kupitisha matumizi ya bajeti ya Sh Bil 10.2 kwa Wakala wa Maji safi na Usafi wa Mazingira RUWASA katika halmashauri hiyo ili kukamilisha utekelezaji wa Miradi mbalimbali inayojengwa na Wakala hiyo.

Akizungumza katika kikao cha baraza la Madiwani kilichofanyika katika Ukumbi wa Halmashauri Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri ya Msalala Khamis Katimba amesema kuwa,kutokana na michango ya Madiwani ndani ya Kikao cha baraza hilo ni ishara tosha kwamba wameridhishwa na umahiri wa watendaji wa RUWASA hasa katika utekelezaji wa Miradi mbalimbali ya Maji katika maeneo mbalimbali ya Halmashauri hiyo.

Kimsingi jukumu la Madiwani ni kuhamasisha jamii kushiriki katika shughuli za maendeleo ikiwemo kuibua Miradi ya maendeleo katika maeneo yao na kupatiwa taarifa namna  Serikali inavyotoa fedha kwa ajili ya Miradi mbalimbali pamoja na matumizi na ushirikishwaji wa wananchi katika kuilinda na kuzuia uharibifu wa miundombinu.

Mkurugenzi huyo aliwataka wananchi kuilinda miundombinu hiyo kwa sababu Miradi hiyo inafaida kwao na kwamba Serikali chini ya Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. Samia Suluhu Hassan imejikita kuhakikisha inamtua mama ndoo kichwani na kwamba wananchi wameshushudia Miradi mingi ya maji ikitekelezwa kwenye Halmashauri hiyo.

“Lengo la Serikali kuweka Miradi hiyo ni kwa ajili ya kuhakikisha inaboresha mazingira ya upatikanaji wa maji kwa wananchi hivyo niwashauri wananchi muitunze Miundombinu hiyo ili iweze kukaa muda mrefu na wananchi wanufaike na Miradi hiyo,hivyo ninyi waheshimiwa Madiwani mnajukumu la kuhakikisha miundombinu ya Miradi yote ya maji inatunzwa na si vinginevyo,” alisema Katimba.

Kikao cha Baraza la Madiwani wa Halmashauri ya Msalala kilifanyika katika Ukumbi wa Mikutano wa Halmashauri hiyo huku Mkurugenzi huyo akitoa Onyo kali kwa wafugaji na kuwataka kuwa makini na Mifugo yao ambayo imeelezwa kuwa ndiyo chanzo cha uharibifu wa Miundombinu ya barabara katika maeneo mbalimbali nchini.

 “Niwaombe sana ndugu zangu wafugaji,tuhakikishe tunapitisha mifugo yetu katika maeneo maalumu yaliyotengwa wakati wa ujenzi,tuepuke kupitisha mifugo kwenye barabara,lakini pia kwa upande wa wananchi  wanaojishughulisha na shughuli za Kilimo tuache kulima kandokando ya barabara zetu ninyi Madiwani hamasisheni ulinzi wa Miundombinu hii muhimu ya maji pamoja na  barabara,matumizi sahihi ya Miundombinu hii yatatufanya  tufanikiwe kunufaika katika Nyanja za Elimu, Maji na Uchumi ” alisema Katimba.

Akizungumza na waandishi wa Habari waliotaka kujua Siri ya mafanikio yaliyopelekea Wakala hiyo kupongezwa na Madiwani wa Msalala Kaimu Meneja wa Wakala wa Maji Safi na Usafi wa Mazingira Vijiji (RUWASA) Wilaya ya Kahama Pastory Mnyeti alisema kuwa,siku hiyo baraza la Madiwani lilikaa kwa ajili ya bajeti kwa upande wa wadau kwa maana ya RUWASA na TARURA ambao wamewasilisha kwa ujumla mpango na bajeti kwa mwaka wa fedha 2024/2025.

Mnyeti alisema kuwa mapendekezo ya bajeti yalifanyika kwa kushirikisha   Madiwani ambao ndiyo wadau muhimu na ambao ndiyo wanaokaa karibu zaidi na wananchi lakini pia ndiyo wanaojua mahitaji ya wananchi wao hatua ambayo RUWASA imepongezwa na Madiwani hao kwa utekelezaji wa Miradi ya maji katika maeneo yao.

“Sisi RUWASA bajeti yetu imejikita katika Miradi inayoendelea,ili tuhakikishe inakamilika kwa wakati na kwamba Miradi hiyo tuhakikishe inatoa huduma ya maji safi na salama kwa wananchi kwa wakati lakini pia kwa Miradi mipya pamoja na kuendelea kufanya Utafiti wa maji chini ya Ardhi ili kuweza kupata vyanzo vipya vya maji kuongeza ufanisi katika usimamizi wa Rasrimali za maji”alisema Kaimu Meneja huyo wa RUWASA.

Aidha Kaimu Meneja wa RUWASA Pastory Mnyeti alimshukuru Rais Dkt Samia Suluhu Hassan kwa kuendelea kuwapatia fedha kwa ajili ya utekelezaji wa Miradi bora ya maji lengo likiwa ni kuhakikisha wanaondoa changamoto ya upatikanaji wa huduma ya maji safi na salama kwa wananchi ili waweze kuendelea na shughuli zao za kiuchumi katika maeneo yao.

Kuhusu bajeti ya mwaka 2024/2025 Kaimu Meneja wa Wakala wa Maji safi na Usafi wa Mazingira Pastory Mnyeti alisema kuwa wamependekeza kutumia kiasi cha shilingi Bilioni 10.2 ili kupunguza changamoto katika maeneo yote ya Miradi iliyoainishwa na kwa Miradi inayoendelea na kwamba kwa kipindi cha 2023/24 RUWASA ilitengewa kiasi cha shilingi Bilioni 5.3 ambapo mpaka kufikia Disemba mwaka 2023 walipokea bilioni 2.7 na kwamba ndizo zinazoendelea kutumika mpaka sasa katika Miradi ya maji.

Naye Diwani wa Kata ya Mwakata Siksi Ibrahimu alimtaka Kaimu Meneja wa RUWASA Pastory Mnyeti kuendelea kujituma kwa kushirikisha Madiwani wa maeneo husika,huku akibainisha kuwa kiini cha RUWASA kupongezwa na Madiwani kumetokana na maandalizi mazuri ya Taarifa yake aliyoiandaa ambayo inaakisi uhalisia.

“Niwashukuru sana watendaji wa Wakala wa maji safi na usafi wa Mazingira RUWASA sisi Madiwani kila mmoja wetu amemsikiliza vizuri Kaimu Meneja,amezungumza vizuri na tumeelewa vizuri,Mhe. Mwenyekiti mpaka muda huu wewe mwenyewe ni shahidi umewaona Madiwani wameridhika na kikao kimetulia”alisema Diwani huyo.

Katika hali ambayo imezoeleka ni kwamba mara nyingi katika Vikao kama hivyo Madiwani wasiporidhishwa na jambo lolote hupaaza Sauti kupinga kinachosemwa na watendaji wa Serikali lakini kutokana na taarifa ya Kaimu Meneja wa RUWASA Pastory Mnyeti,Madiwani wamekiri kuwa taarifa hiyo imesheheni ukweli na hawana sababu ya kuikosoa wala kuipinga.

“Vikao kama hivi sisi Madiwani tusiporidhishwa na jambo lolote huwa tunajipanga kupaaza Sauti kupinga kinachosemwa na watendaji wa Serikali,lakini kutokana na taarifa ya Kaimu Meneja wa RUWASA Madiwani wote  tunakiri kuwa taarifa hiyo  imesheheni ukweli na hatuna sababu ya kuikosoa wala kuipinga”alisema Mh Diwani huyo.


Post a Comment

Mpya zaidi Nzee zaidi